TIMU ya Mbeya City inayomilikiwa na Halmashauri
ya Jiji la Mbeya, imetangaza kujiondoa rasmi kwenye mbio za ubingwa wa
Ligi Kuu Bara msimu huu baada ya kuanza vibaya kwenye mechi saba na
akili zote sasa wamezielekeza katika kuiokoa timu hiyo na janga la
kushuka daraja.
Katibu Mkuu wa timu hiyo, Emmanuel Kimbe, alisema
kwa sasa hawana ndoto za kutwaa ubingwa ama kumaliza kwenye nafasi za
juu kama msimu uliopita, hivyo wanajipanga kuhakikisha timu inabaki Ligi
Kuu na ndipo mipango mingine iendelee.
Mbeya City ilifanya vizuri msimu uliopita na
kufanikiwa kumaliza katika nafasi ya tatu lakini imeanza vibaya msimu
huu baada ya kushinda mchezo mmoja pekee kati ya saba huku ikiwa
imefungwa mechi nne na kuishia kushika mkia kwenye msimamo wa ligi ikiwa
na pointi tano.
“Tumejiondoka rasmi kwenye mbio za ubingwa, kwa
sasa tumeweka akili zote katika kuhakikisha timu inasalia Ligi Kuu kwani
ikishuka daraja itakuwa ni majanga,” alisema.
“Kuhusu taarifa za kocha Juma Mwambusi kujiuzulu
bado hatujapokea barua rasmi, jana (Juzi Jumamosi) haikuwa siku ya kazi,
leo pia (Jana Jumapili) siyo siku ya kazi, nadhani kesho (leo Jumatatu)
tutakuwa kwenye nafasi nzuri ya kulizungumzia.
“Kama kajiuzulu kweli tutafanya utaratibu wa kupata kocha mwingine.”
No comments:
Post a Comment